Skip to main content

KWA NINI SHERIA MPYA YA HABARI NI MUHIMU ZANZIBAR

 


NA NAFDA HINDI, ZANZIBAR

Ni takriban miaka 20 sasa, shauku ya waandishi wa habari pamoja na watetezi wengine wa haki za binaadamu Zanzibar kuona nchi yao inapata sheria rafiki za habari imekuwa ikitimizwa kwa maneno. Viongozi wa ngazi mbalimbali serikalini wamekuwa wakitoa ahadi lakini utekelezaji wake unasuasua.

Tangu alipoingia madarakani, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi, amekuwa akionesha kutambua umuhimu wa sekta ya habari kusimamiwa kwa kutumia sheria zilizo rafiki, kwa vile si mkosefu wa kujua ukweli kuwa sheria zilizopo ni kongwe zisizoendana na mazingira mapya yanayochagizwa na kasi ya ukuaji wa sayansi na teknolojia.

Akiwa amekalia kiti cha Ikulu baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2020, Dk. Mwinyi hakuchukua muda kusikika akitoa matamshi yenye mtizamo wa kupendelea waandishi wawe na uhuru zaidi wa kufanya kazi zao, kwa kuamini kuwa itarahisisha manufaa ya utendaji wao kuwafikia wananchi kwa ukamilifu.

Mara baada ya Baraza la Habari Tanzania (MCT) kutoa ripoti ya utendajikazi wa vyombo vya habari, mwaka 2021/2022, ikieleza kuwa Zanzibar inahitaji sheria “mpya kabisa” za kusimamia sekta ya habari, Serikali ilijikuta inakumbushwa jukumu au wajibu wa kufanyia kazi suala hilo kwa kuwa limepigiwa kelele muda mrefu. Harakati za waandishi na wadau kutaka mageuzi ya sheria zilianza mwaka 2002.

Ni hapo, Rais Dk. Mwinyi alipojibu kutambua “sheria za habari za Zanzibar ni za muda mrefu na Serikali anayoiongoza ipo tayari kushirikiana na wadau wa habari, kuzifanyia kazi kulingana na mapendekezo yatakayotolewa.” Alisema, “pendekezo lenu la kwamba Zanzibar imefika wakati wa kupata sheria nzuri, tutalifanyia kazi.”

Ilipofika mwaka 2023, kwenye kilele cha maadhimisho ya Siku ya Uhuru wa Vyombo vya Habari Mei 3, Rais Mwinyi aliiambia hadhara kwamba serikali yake itaendelea kuheshimu na kuthamini haki ya uhuru wa habari na kujieleza. Maadhimisho yalifanyika kwenye ukumbi wa Hoteli ya Golden Tulip Uwanja wa Ndege.

“Serikali zote mbili zitaendelea kushirikiana kwa karibu na vyombo vyote vya habari katika kuhakikisha serikali inatatua changamoto zinazowakabili wanahabari,” alisisitiza.

Mbele ya Rais, Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo wa Zanzibar, Tabia Maulid Mwita, akikazia muelekeo wa Rais, alisema mchakato wa sheria ya habari Zanzibar umefikia asilimia 80 kukamilika na akasihi wadau wa habari kuendelea kuwa na subira.

“Serikali yenu ni sikivu, tunawahakikishia kuwa na sheria nzuri zitakazokidhi matakwa ya sasa, tutawasilisha Baraza la Wawakilishi na taratibu nyingine ziendelee,” Waziri Tabia alisema.

Kuonesha kuwa serikali inakumbuka kilio cha waandishi wa habari kutaka sheria rafiki za kusimamia sekta ya habari, na kwamba haijasahau wajibu wake wa kuona hilo limetimia, serikali ilirudia msimamo wake wakati wa maadhimisho ya siku ya uhuru wa vyombo vya habari duniani Mei mwaka huu.

Katika maadhimisho yaliyoandaliwa na kuratibiwa na serikali kupitia Wizara ya Habari, tarehe 4 Mei, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Fatma Rajab akimwakilisha Waziri Tabia, alisema “Serikali itahakikisha mageuzi ya sera na sheria za habari nchini yanaenda sambamba na kanuni pamoja na maadili ya vyombo vya habari.”

Kauli hiyo ilizingatia kauli mbiu ya kitaifa ya wadau wa habari Zanzibar ya mwaka huu 2024, iliyosema: Uhuru wa Vyombo vya Habari. Mageuzi ya Sera na Sheria za Habari Zanzibar.”

Kaulimbiu hii ilitiliwa mkazo na mantiki yake kufafanuliwa vizuri Mei 23 mwaka huu wakati wa wadau wa  taasisi za habari na washirika wao katika utetezi wa haki za binaadamu, lilipoalika watu mbalimbali kwenye maadhimisho waliyoandaa na kukaribisha Katibu Mkuu, Fatma kuwa mgeni rasmi. Alimtuma Katibu Mtendaji wa Tume ya Utangazaji Zanzibar, Suleiman Abdalla ambaye alisema:

“Kwa sasa sheria ya habari, ipo kwa Mwanasheria Mkuu wa serikali na tunatarajia hivi karibuni itapelekwa Baraza la Wawakilishi kama muswada na tunaomba walioko huko waichangie vizuri ili iweze kupita na kupatikana sheria mpya.”

 

Ni kwanini waandishi wa habari watoe kilio chao cha kutaka mageuzi ya sheria za habari? Analo jibu Dk. Mzuri Issa, Mkurugenzi wa Chama cha Waandishi wa Habari Tanzania (TAMWA-ZANZIBAR). “Haiwezekani kuwa na sheria za udhibiti mpaka sasa, ukitaka kufanya usajili wa gazeti lazima Waziri aamue, asipotaka huwezi (kusajili). Katika mazingira haya hatuwezi kwenda kwa wakati huu tunapozungumza utawala wa demokrasia.”

Utambuzi wa uhuru wa vyombo vya habari, unaanzia Umoja wa Mataifa ambako mwaka 1948 Baraza lake la Usalama lilipitisha azimio lililojenga msingi wa imani kwamba ni muhimu haki na uhuru wa vyombo vya habari ikijumuisha uhuru wa kupata habari na ule wa watu kujieleza, ukaheshimiwa na kulindwa. Ibara ya 19 ya tamko hilo la kilimwengu inaelekeza hivyo.

Kiutaratibu, baada ya azimio hilo, kilichofuata ni kwa kila nchi mwanachama wa umoja wa mataifa, kuridhia kwa kusaini azimio; na kupitia bunge lake, itunge sheria ya kutambua mantiki na kujipa dhima ya kusimamia utekelezaji wa azimio kulingana na mazingira iliyoko.



Zanzibar baada ya kuungana na Tanganyika, maslahi yake katika suala hilo yakabebwa na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo iliridhia azimio na kupaswa kutunga sheria ya kuchukua dhima ya kulitekeleza. Zanzibar ilikuja kutambua rasmi haki na uhuru wa habari ilipoandika katiba yake ya pili mwaka 1984 baada ya kufutwa kwa Katiba ya Kwanza ya mwaka 1963 na kuweka dhima katika Ibara ya 18.

Miaka minne baadaye, yaani mwaka 1988, ilitunga sheria ya kwanza iliyoiita Sheria ya Usajili wa Wakala wa Habari, Magazeti na Vitabu Na. 5 ya mwaka 1988. Ikapata marekebisho ya kwanza kupitia Sheria Na. 8 ya mwaka 1997. Sheria nyingine maarufu ni iliyohusu utangazaji ambayo ni Sheria ya Tume ya Utangazaji Zanzibar Na. 7 (1997), na yenyewe ikiwa imerekebishwa kwa Sheria Na. 1 (2010).

Ni msimamo wa waandishi na taasisi za kibahari kwamba sheria hizi haziendani na mazingira ya sasa. Ni kongwe zinazopingana na dhamira na dhima ya kuheshimu na kulinda haki na uhuru wa habari. Sheria hizi zinatajwa kuzorotesha wananchi kufaidika na uhuru unaokusudiwa na umoja wa Mataifa.

Kwa mfano, kifungu cha 27(2) cha Sheria ya Usajili wa Wakala wa Habari, Magazeti na Vitabu Na. 5 (1988) iliyorekebishwa kwa Sheria Na. 8 (1997), kinasema: “Hakimu yeyote anaweza kutoa hati kumuidhinisha Afisa wa Polisi yeyote, wa cheo cha Inspekta kwa msaada au bila msaada, kuingia na kupekuwa mahali popote pale inaposhukiwa kuwa kuna gazeti linachapishwa kinyume na sheria hii, au kanuni zozote zililotungwa, ama limefanya au linafanya au linakaribia kufanya kosa, hivyo anaweza kukamata gazeti lolote linalopatikana humo ama kwa kushuku kuwa kuna gazeti lililochapishwa au linachapishwa pamoja na ushahidi mwengine wowote kwa kutenda kosa chini ya sheria hii, au kanuni zozote zilizopo zitakazopatikana”.

Kwa muktadha huo, kifungu cha maneno yaliyotumika yana utata ndani yake. Hayaeleweki sawasawa kwa sababu kimekusanya maneno mengi na tata yasiyofahamika, na dhana ya kushuku tu inamruhusu Polisi kuingia kwenye ofisi ya gazeti, kupekuwa, na akijiridhisha tu na shuku yake, anaweza kukamata au kuzuia gazeti husika kuchapishwa.

 Ni imani ya waandishi wa habari na watetezi wa haki za binaadam kuwa uandishi wa habari, ni fani  kama zilivyo udaktari, uhandisi, uuguzi, uanasheria na ualimu, ni kazi ya kitaaluma. Je ofisa wa polisi anaijua taaluma inavyoelekeza? Je, dunia ingali kwenye wakati wa kuendesha mambo kwa kushuku?

Hawra Shamte, mwandishi mwandamizi nchini, akigusia ubaya wa kifungu hicho, anasema: “Kinampa mamlaka Hakimu atowe kibali kwa Inspekta wa polisi kupekuwa jengo kwa kushuku tu ikiwa sehemu hiyo inachapishwa gazeti linalokwenda kinyume na taratibu labda za maadili ya nchi, mila na desturi au kuhatarisha amani na utulivu.”




“Hichi kifungu hakiko sawa na kina dalili za ukandamizaji wa uhuru wa habari kwa sababu hatwendi kwa dhana na shuku. Tunashauri kirekebishwe kwa maslahi ya nchi na wananchi,” anasema. Pia anatanabahisha kuwa sheria yenyewe haikueleza maana ya “maadili ya nchi, mila na desturi au kuhatarisha amani na utulivu.”

Malalamiko pia yanaihusu Sheria ya Tume ya Utangazaji Zanzibar Na. 7 (1997), na marekebisho yake kupitia Sheria Na. 1 (2010), kwamba inawapa viongozi wa serikali mwanya wa li kuingilia shughuli za utangazaji ambazo kimantiki ya azimio la Umoja wa Mataifa, zinapaswa kufanywa kwa uhuru mpana.

Mwandishi mwandamizi wa habari nchini, Jabir Idrissa, anasema: “Sheria hii inaipa nguvu Tume ya Utangazaji, kufungia na kufutia leseni vyombo vya utangazaji, hivyo kwenda kinyume na viwango vya kimataifa vinavyoitaka tume kuwa huru na inayojitegemea.”

Mwanasheria na Mkufunzi wa Chuo Kikuu cha Zanzibar (ZU), Said Ali, anasema Sheria ya Tume ya Utangazaji, inatoa mamlaka makubwa kwa viongozi serikalini kuchukuwa maamuzi yoyote anayoona yanafaa kwa kisingizio cha amani na utulivu ingawa haikufafanuliwa tafsiri yake rasmi kwenye sheria.

“Kifungu 27(2), Waziri amepewa mamlaka makubwa ya kuchukua maamuzi yoyote, mfano kama ana tofauti binafsi na mtu fulani ambae ni mmiliki wa chombo cha habari, anaweza akaitumia sheria hii vibaya na kumtia hatiani mtu huyo kwa kufungia chombo hicho cha habari."

Uzoefu unaonesha kuwa kiongozi anaweza kuamka na matatizo yake binafsi na kwa kuwa anayo mamlaka ya kisheria, akayatumia hayo vibaya kwa kutoa amri dhidi ya ustawi wa uhuru wa habari, akasababisha chombo kufungwa na hivyo kukwamisha manufaa yanayotarajiwa na umma.




Najjat Omar ni mwandishi wa habari ambaye anahofia kuendelea kwa Sheria ya Tume ya Utangazaji Zanzibar, kutasababisha waandishi kutofanya kazi kwa uhuru na weledi kwa vile wanagubikwa na woga. Kwa hapo, watashindwa kutimiza wajibu wa kuishauri serikali kuhusu kudhibiti watumishi wake wanaozuia taarifa muhimu kwa kisingizio cha kulinda maslahi ya usalama wa taifa, ambayo hayajafafanuliwa katika sheria.

“Hatutoweza kuwawajibisha wanaokula fedha za umma tofauti na matarajio ya serikali, muhusika anaweza kusema mradi huu umetumia shilingi milioni mia moja kumbe tathmini inaonesha matumizi sahihi ni shilingi milioni 20. Mwandishi akikaa kimya kufumbia uovu huo, na mtumishi mwengine atapiga milioni mia mbili,” anasema Najjat.

Mwanasheria Shadida Omar kutoka Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binaadamu Tanzania (THRDC), anasema ili kuona uhuru wa kujieleza unafanikiwa kwa manufaa ya jamii, waandishi wanadhima ya kupaza sauti kwa kupata sheria mpya ya habari inayokwenda na mabadiliko ya dunia ya sasa.

“Hapa kwetu Zanzibar zipo sheria nyingi zinabadilishwa mara kwa mara na katika muda mfupi, inashangaza hizi sheria zinazohusu sekta ya habari zinacheleweshwa wakati inajulikana wazi kuwa ni za zamani zinazokwaza uhuru wa habari,” anahoji.

Mwanasheria huyo anaitaja mojawapo kuwa ni Sheria ya Uchaguzi Zanzibar, Na. 11 ya mwaka 1984 ambayo imerekebishwa kupitia Sheria Na. 4 ya mwaka 2017. Sasa inaitwa Sheria ya kufuta Sheria ya Uchaguzi Na. 11 ya mwaka 1984 na kutunga Sheria ya Uchaguzi ya mwaka 2017 na masuala mengine yanayohusiana nayo. Sheria hii mpya ilisainiwa na Januari 16, 2018.

Mshauri Elekezi na Mwalimu wa Uandishi wa Habari Tanzania na Afrika Mashariki, Salim Said Salim anasema demokrasia sahihi hutegemea “sana” uhuru wa vyombo vya habari katika nchi, kwa sababu vyombo vya habari vina dhima ya kuchangia maendeleo ya nchi kwa kupaza sauti na kuwawajibisha viongozi wanaotumia mamlaka kinyume cha sheria.

“Hii Sheria ya Habari ina miaka takriban 20 sasa tokea kuanza kuilalamikia, tunapewa ahadi kila siku lakini bado hatujaona utekelezaji wake. Kama ni mtoto tayari angekuwa anasoma chuo kikuu,” anasema veterani aliyeanza kuwa mwandishi wa habari mwaka 1965.

Mwenyekiti wa Kamati ya Habari Zanzibar (ZAMECO) ambaye pia ni Mwenyekiti wa Klabu ya Waandishi wa Habari Zanzibar (ZPC), Abdalla Mfaume anasema jitihada zinahitajika kwa waandishi kuendelea kudai sheria mpya ya habari itakayotoa fursa kwa wote kupata haki bila ya ubaguzi na kuleta maendeleo katika nchi.

Mfaume anaimarisha hoja ya Dk. Mzuri anayeamini kampeni ya kupigania sheria mpya za habari lazima iendelee. Anasema, “Tumewahi kuzungumza na Mhe. Rais kuhusu sheria hizi, na Waziri (wa Habari) pia, nadhani inabidi tupange kuzungumza nao tena ili tuone hili linakwendaje. Haitapendeza hata kidogo kumaliza mwaka huu (2024) hatujapata mabadiliko ya sheria za habari.”

Msimamo huu aliutoa katika tamati ya maadhimisho ya Mei 23 baada ya kusikiliza kauli za viongozi wa serikali kuwa mara mapendekezo yapo kwa kamati ya makatibu wakuu, mara kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali mara imerejeshwa kwa mwanasheria ili kutafsiriwa kwa Kiswahili.”

MWISHO.

Comments

BLOG'S VISITORS

DAKTARI MWENGINE CHAKE CHAKE KULA SIKUKUU POLISI, NI KWA TUHUMA ZA KUMBAKA MGONJWA WAKE

NA WAANDISHI WETU, PEMBA::: DAKTARI anaetoa huduma kwa wagonjwa kituo cha afya cha serikali cha  Gombani wilaya ya Chake Chake Pemba, Is-haka Rashid Hadid, anaendelea kushikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa kaskazini Pemba, akituhumiwa kumtorosha na kisha kumbaka mtoto wa mwenye umri wa miaka 16, mkaazi wa Gombani. Daktari huyo miaka 35 ni mkaazi wa Kangagani Wilaya ya Wete mkoani humo, ambapo anadaiwa alimchukua mtoto huyo kutoka kwa rafiki yake, na kumpeleka kwenye nyumba anayoishi eneo la Kangagani. Mtoto aliefanyiwa kitendo hicho alisema kuwa, April 21 mwaka huu alikwenda kituo cha afya Gombani, kwa ajili ya matibabu na baada ya kupatiwa huduma na daktari huyo, alimuomba nambari yake ya simu. Alisema ilipofika usiku, walikuwa wanawasiliana kupitia ujumbe mfupi (sms) kwa lengo la kwenda kuchukua dawa nyingine ambazo kwa mchana huo alizikosa hospitalini hapo. "Nilikwenda hospitali kutibiwa, baada ya kufanya mapele katika sehemu zangu za siri, lakini akaniambia mpaka aje da

'MKAPA' NA WENZAKE PEMBA WALAZWA RUMANDE

  NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@ MAHKAMA kuu Zanzibar kisiwani Pemba, chini ya Jaji Ibrahim Mzee Ibrahim, imewapeleka rumande watumuhimwa wanne wanaokabiliwa na tuhuma za kuua kwa makusudi, akiwemo Ali Mussa Omar ‘ Mkapa’ mkaazi wa Wawi wilaya ya Chake chake Pemba. Watuhumiwa wengine walioanza maisha mapya ya rumande ni mtuhumiwa Yassir Mohamed Juma miaka 23, Anuwari Mussa Omar miaka 30 pamoja na mtuhumiwa Yassir Mussa Omar ‘ Makababu ’ miaka 29, wote wakaazi wa shehia ya Wawi, wilaya ya Chake chake Pemba. Awali watuhumiwa hao waliwasili mahakamani hapo, kwa mara ya kwanza, kwa ajili ya kusomewa tuhma zinazowakabili za kumuua kwa maksudi Said Seif Kombo. Ilidaiwa mahakamani hapo na Mwendesha Mashtaka kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashataka Seif Mohamed Khamis akiambatana na mwenzake Mussa Khamis Ali kuwa, watuhumiwa hao kwa pamoja wanadaia kufanya mauwaji hayo kwa maksudi. Ilidai kuwa, watuhumiwa wote kwa pamoja, walitenda kosa hilo Oktoba 16, mwaka huu, baina ya saa 7:00 mchan

HII KALI MBUNGE ASIYA AMKOGESHA MWANANCHI HADHARANI KISA HICHI HAPA......

  NA HAJI NASSOR, PEMBA MBUNGE wa viti maalum nafasi za wanawake mkoa wa kaskazini Pemba Asiya Sharif Omar, amewataka wananchi wa kijiji cha taifu, shehia ya Kinyasini jimbo la Gando wilaya ya Wete Pemba, kuyalinda miundombinu ya maji safi na salama, ili yawe endelevu kwao. Kauli hiyo ameitoa wakati alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi, mara baada ya kuwasili kijijini humo, na kumkogesha mwananchi mmoja kama ishara ya uzinduzi wa mradi wa maji safi na salama, ulioasisiwa na mbunge wa Jimbo la Gando. Alisema, hawana mbadala kwa sasa bali ni kuilinda miundombinu ya huduma hiyo, hasa baada ya mbunge wa wao Salim Mussa Omar, kuwarejeshea huduma hiyo. Alieleza kuwa, inafahamika kuwa kwa miaka 14 waliikosa huduma hiyo hasa kwa vile viongozi waliokuwepo hawakujali kuwatatulia tatizo hilo, hadi juzi ilipofanywa na mbunge wao. “Baada ya huduma hii sasa kurejeshwa na mbunge wa jimbo la Gando, kazi iliyobakia kwenu wananchi ni kila mmoja kuwa mlinzi wa miundombinu hii,’’ali

…….SUZA WATOA USHAURI WA ADHABU YA KUNYONGWA

  NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@ WANAFUNZI wanaosomea uwalimu Chuo cha taifa cha Zanzibar ‘SUZA’ kampasi ya Benjamin Wiliam Mkapa Wete Pemba, wamependekeza adhabu ya kunyongwa hadi kufa, kwa mtu atakaetiwa hatiani, kwa kosa la dawa za kulevya. Walisema, haiingii akili kuona, mahkama imeshamtia hatiani mtu kwa kukutwa na dawa za kulevya, ambazo huathiri nguvu kazi ya taifa na kisha, kupewa hukumu ya kifungo pekee. Wakizungumza leo Juni 26, 2024 kwenye kongamano la vyuo vikuu, juu ya masuala ya msaada wa kisheria, kuelekea wiki ya msaada wa kisheria Zanzibar, lililofanyika Chuoni hapo, walisema wakati umefika sasa kutolewa kwa hukumu hiyo. Walipendekeza kuwa, ni vyema kwa mtu anayetiwa hatiani asibakie chuo cha Mafunzo pekee kuitia tena hasara serikali kwa chakula na wakati mwingine matibabu, wakati tayari ameshasababisha madhara, kwa vijana. Mshiriki Juma Nafasi Juma, alifafanua kuwa kama mtu ameamua kuliumiza taifa kwa kuingiza, kusafirisha, kusambaaza dawa za kulevya, hivyo ni vy

TUHMA ZA DAKTARI PEMBA KUCHIWA HURU: POLISI KASKAZINI KUTOA TAARIFA RASMI LEO

  NA HAJI NASSOR, PEMBA KAMANDA wa Polisi mkoa wa kaskazini Pemba, Juma Saad Khamis, amesema leo Mei 9, mwaka huu atatoa taarifa rasmi, juu ya kuendelea kumshikilia au kumpa dhamana ya Polisi, daktari wa Kituo cha Afya Gombani Is-haka Rashid Hadid, anayetuhumiwa kwa ubakaji. Alisema, kwa vile alikuwa katika mapumziko mafupi, haelewi jambo lolote linaloendelea kwa mtuhumiwa huyo, juu ya kuendelea kushikiliwa kwake kituoni hapo. Alieleza kuwa, leo Mei 6 (jana), hajapata taarifa za ndani za mtuhumiwa, huyo na kuwataka wananchi na wanaharakati, wasubirie hadi Jumatatu ijayo. Akizungumza na waandishi wa habari kwa nyakati tofauti Kamanda huyo, alisema hana taarifa zozote za kupewa dhamana mtuhumiwa ndani ya kituo chake cha Polisi au kuendelea kuwepo. ‘’Ilikuwa mimi sipo kazini kwa muda, kuanzia anakamatwa hadi anafikishwa Polisi, kwa sasa siwezi kueleza jambo lolote kwa mtuhumiwa huyo, hadi Jumatatu,’’alieleza. Aidha Kamanda huyo alieleza kuwa, kwa sasa hawezi kutoa ufafan