Skip to main content

SHERIA ZIZINGATIE UWIYANO WA KIJINSIA ILI KUWAWEZESHA WANAWAKE KIUONGOZI

 



NA HAJI NASSOR, PEMBA::::

MAPUNGUFU yaliyopo katika sheria mbali mbali Zanzibar, zimetajwa kuwa zinachangia kutokuwepo kwa uwiano wa usawa wa kijinsia, kati ya wanawake na wanaume katika ngazi mbali mbali za uongozi.

 

Mapungufu ya sheria hizo yameibuliwa na wanajamii kufuatia mikutano 41 iliyofanyika katika shehia 44 kisiwani Pemba, iliyoandaliwa na wahamasishaji jamii kwa  kushirikiana na asasi za kiraia kisiwani hapa, juu ya ushiriki wa wanawake katika kushika  nafasi za uongozi na demokrasi.

Akizungumza kwenye mkutano na waandishi wa habari juu ya mapungufu yaliyobainika kwenye sheria kukwaza ushiriki wa wanawake kwenye nafasi za uongozi, Mkurugenzi wa Jumuiya ya utetezi wa Jinsia na Mazingira Pemba (PEGAO) Hafidh Abdi August 8, mwaka 2022, alisema miongoni mwa Asasi zilizoshirikiana kuchambua mapungufu hayo ni pamoja na taasisi ya Tumaini Jipya Pemba (TUJIPE), Nihurumie Foundation, KOK Foundation, PRADO, PACSO, Jumuiya ya Wanawake wa Kiislamu, pamoja na Kituo cha huduma za Sheria Zanzibar ZLSC kisiwani Pemba.

 

Alisema hadi sasa nafasi za wanawake ni ndogo kwenye uongozi, na dhamira ni kufikia usawa wa 50 kwa 50 kwa wanawake na wanaume ili usawa ufikiwe, inaonekana kuzorota.

“Katika Wawakilishi wa majimbo 50 wanawake ni  wanane (8)  tu sawa na asilimia 16, Wabunge wa Jamhuri ya Muungano kutoka Zanzibar kwenye majimbo 50 wanawake ni  wannne tu (4) sawa na asilimia nane (8), Mawaziri ni sita sawa na asilimia 33 na Makatibu wa kuu ni saba sawa na asilimia 39.

Kwa upande wa Wakuu wa Mikoa mwanamke ni mmoja tu sawa na asilimia 20, Wakuu wa Wilaya ni wanne sawa na asilimia 36 na Masheha wanawake ni 68 sawa na asilimia 17 kwa masheha wote ambao ni 389,” alisema.

 

Alitaja miongoni mwa sheria zilizoonekana kuwa na mapungufu ni pamoja na Sheria ya Uchaguzi Nambari 4 ya 2018 ambapo licha ya kwamba Sheria hiyo inasimamia na kutoa muongozo mzuri wa jinsi ya kupatikana kwa wagombea na viongozi wa nchi, lakini bado ipo kimya katika kueleza utaratibu wa kupatikana kwa wagombea katika hatua za awali kupitia vyama vyao hasa ikizingatiwa kila chama kuwa na utaratibu wake wa upatikanaji wa wagombea. 

Alisema “kutokana na mapungufu katika sharia hiyo, hivyo ni vyema Sheria ikaweka utaratibu rasmi wa kulazimisha upatikanaji wa wagombea wa kila chama kwa kuzingatia usawa wa kijinsia katika kila nafasi.”

 

Pia Sheria ya Utumishi wa Umma Na. /2011 ambayo inayosimamia haki na wajibu wa watumishi wa Umma katika Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, ambapo kifungu cha 18 cha kimeanzisha Kamisheni ya utumishi wa Umma itayoongozwa na Mwenyekiti atakayechaguliwa na Rais pamoja na wajumbe wengine sita watakaochaguliwa na Rais kwa mapendekezo ya kila wajumbe wawili kutoka kwa Waziri husika, Spika wa Baraza la Wawakilishi na Jaji Mkuu, kufanya jumla ya watu 7.

“Lakini kifungu hiki hakikuweka uwiyano wa kijinsia, jambo ambalo ni changamoto inayoweza kusababisha wanaume watupu wakaunda tume hiyo,” aliongeza mkurugenzi huyo.

 

Sheria nyingine ambazo zimebainika kukwaza uwiano wa ushiriki wa wanawake katika nafasi za uongozi ni Sheria ya Watumishi wa Umma Kushiriki Katika Siasa Sheria Na. 3 ya mwaka 2003Sheria ya Elimu ya mwaka 1982, Sheria ya Mahakama ya Kadhi Namba 9/2017, Pamoja na Sheria ya Usimamizi wa Mahakama, Na. 11/2018.

Katika hatua nyingine alibainisha kuwa mkataba wa Kimataifa wa kutokomeza  aina zote za ubaguzi dhidi ya wanawake (CEDAW) wa mwaka 1979 ambapo unazitaka nchi zote wanachama ambazo zimeridhia mkataba huo ikiwemo Tanzania, kutekeleza wajibu mahsusi katika kuhakikisha wanawake wanapata haki zote za binadamu kwa usawa, kuondoa aina zote za ubaguzi dhidi ya wanawake bila ya kujali hadhi yao kindoa.


Alifahamisha kuwa “sambamba na hilo pia mkataba huo unasisitiza upatikanaji wa haki za msingi za binadamu kwa usawa katika nyanja za kisiasa, kiuchumi, kijamii, kiutamaduni, kiraia na nyinginezo, pamoja na kuweka usawa kati ya wanawake na wanaume katika mfumo wake wa kisheria na kitaasisi.”

 


Aidha kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar ya 1984 kifungu cha 11(1) kinaeleza kwamba binadamu wote huzaliwa huru na wote ni sawa,  kifungu cha 12 kinazungumzia suala la haki ya usawa mbele ya sheria kuwa watu wote watakua sawa mbele ya sheria na wanazo haki sawa mbele ya sheria bila kubagua jinsi, dini, rangi na asili ya mtu.

 

Licha ya changamoto mbalimbali zilizoko katika sheria hizo juu ya nafasi ya mwanamke, ziko sheria ambazo zimetambua nafasi ya mwanamke katika mambo mbali mbali kama vile Sheria ya Mahakama ya Kadhi Namba 9/2017 Kifungu cha 5(1)(f) ambacho kimewapa nafasi wanawake katika kupeleka malalamiko yao juu ya ugawaji wa mali.

“Hii ingesaidia kuondosha uonevu wa muda mrefu na umasikini kwa wanawake, ambao mara nyingi huachwa na kunyang’anywa kila kitu, na hivyo inamlazimu kuanza upya maisha pamoja na nguvu nyingi alizotupa katika kutengeneza utajiri wa familia,’’alieleza.

Hata hivyo, alisema tunasikitika kuwa manufaa haya hayapati mwanamke kwani bado utekelezaji wake unafuata matakwa ya kadhi muhusika kwa vile haijaelezwa bayana kwenye sheria kuwa mchango na siyo lazima wa kutoa pesa na kuwa na risiti lakini hata ule wa hali na usio wa pesa ukiwemo wa kushughulikia nyumba, watoto, baba, wazee na wagonjwa wakati mwenza yuko kazini.”

 

Pia Sheria ya Ajira namba 11/2005 imetoa ulinzi mzuri wa wanawake juu ya masuala mbali mbali ya utumishi wa umma kifungu cha 10 (2) kinaeleza kwamba muajiri analazimika kuchukuwa hatua ya kutoa fursa sawa katika sehemu ya kazi na kuondoa ubaguzi katika sera yake na utendaji wake, kuthibitisha kuwepo kwa malipo sawa ya mishahara kwa mwanamke na mwanamme kwa kazi ya aina moja,

“Suala jengine lililokatazwa na kukemewa katika Kifungu cha 11 cha sheria hii ni unyanyaswaji wa kijinsia, vitendo vya kumtaka muajiriwa wa kike kimapenzi, matumizi ya vitisho na lugha inayoashiria mapenzi (ngono).

Aliongeza, “Sababu moja ya waajiri wengi kukataa kuwaajiri wafanyakazi wanawake ni kuwa muda mwingi watakuwa hawapo kazini kutokana na kujifungua. Suala ambalo limekatazwa moja kwa moja na Sheria hii. Katika kuhakikisha ya kwamba mwanamke anapata nafasi nzuri ya mapumziko na kulea mtoto wake miezi 3 yenye malipo na akijifunguwa mapacha atapata likizo ya siku mia moja.”

“Aidha ni marufuku kumuajiri mwanamke katika sehemu ambazo zinahusika na kemikali za sumu ambazo zitahatarisha uzazi au mimba ya mfanyakazi huyo kama ilivyoelezwa katika Kifungu cha 84 (4) na Kifungu cha 85 (1)kinkataza  kumpangia kazi mfanyakazi mwanamke wakati wa usiku katika shughuli zozote za viwanda.”

Aidha Sheria ya Elimu  namba 6/1982 katika kifungu cha 19 inaeleza     “Itakuwa ni lazima kwa kila mtoto aliyefikia umri wa miaka saba lakini hajafika miaka kumi na tatu kuandikishwa Elimu za msingi

Alibainisha, “kifungu hiki kinamaanisha kwamba haki ya elimu ni haki ya jamii nzima bila kujali tofauti ya kijinsia, nah ii inamlinda mtoto wa kike pia kwani kuna baadhi ya wanajamii wanakataa kuwapeleka watoto wa kike skuli kupata elimu ambayo itamjenga yeye kuwa kiongozi bora hapo baadae.”



Sheria ya kuwalinda wari na watoto wa mzazi mmoja namba 4/2005 katika Kifungu cha 5 (1) kinaeleza kuwa mwari yeyote, mtoto wa kike, au mwanamke ambaye hajaolewa akipata ujauzito au akijifungua nje ya ndoa  anaweza kufungua kesi ya madai katika Mahakama ya Wilaya kudai matunzo ya mtoto kutoka kwa mtu aliyedhaniwa kuwa ni baba wa mtoto au aliyemsababishia ujauzito, kabla ya kujifungua au wakati wowote kabla ya mtoto hajatimiza umri wa miaka kumi na nane (18) au kabla ya mtoto kuweza kujitegemea mwenyewe. Kifungu hichi kinawasaidia wanawake wale ambao walipata ujauzito bila ya ridhaa yao kama vile kubakwa kuweza kudai haki hizo za mtoto Mahakamani.

“Pia tukiingalia Sheria ya Adhabu namba 6/2018 hii inatoa ulinzi kwa wanawake au watoto wa kike juu ya vitendo vya ubakaji dhidi yao ambapo kifungu cha 108 kimeonesha mazingira hayo na kifungu cha 109 kimetoa adhabu kwa yoyote atakayefanya kitendo hicho kutumikia kifungo cha maisha au kifungo kisichopungua miaka thelathini.

 

 Pia sheria imetoa adhabu kwa kosa la kumtorosha mwanamke au mtoto wa kike ili kumlinda mwanamke na vitendo vilivyo nje ya maadili,” alieleza.

Sheria ya kuanzisha mabaraza ya Vijana Zanzibar namba 16 ya 2013 katika kifungu cha 33 kimesisitiza kuzingatia uwiano wa jinsia katika muundo wa uongozi katika mabaraza hayo, vile vile katika kifungu cha 34(2) kimeonesha uongozi wa baraza la vijana



Ambapo kwa Mwenyekiti na Makamu mwenyekiti, na ikiwa Mwenyekiti ni mwanamme basi Makamu mwenyekiti awe mwanamke au ikiwa Mwenyekiti ni mwanamke basi Makamo mwenyekiti awe mwanamme. Sheria kama hii inapaswa iwe ndio muongozo kwa nyengine.

 

Kutokana na mapungufu yaliyobainika katika sharia hizo, wadau hao wamependekeza mambo mbalimbali.

 

“Pia sheria ya usajili wa vyama vya siasa zirekebishwe ili ilazimishe vyama kuweka asilimia maalum ya wanawake katika kugombea.

 

Aidha pia, “vyama vya siasa viwazingatie na kuwapa vipaumbele wanawake waliojitokeza katika kugombea na kushika nafasi ya kuwa mtu wa pili au kupitwa kwa kura moja tu.” 

Aliongez, “Tunashauri pia sheria zinazotoa haki kwa wanawake zieleweke vizuri kwa nchi nzima ili wanawake waweze kuzidai haki hizo ikiwemo makazini katika kupambania haki zao za kisiasa na kijamii.

Mradi wa kushajiisha ushiriki wa wanawake katika uongozi na demokrasia  ni mradi wa miaka minne (2020 – 2023) wenye lengo la kukuza ushiriki wa wanawake katika uongozi ambao unatekelezwa  na Jumuiya ya Wanasheria Wanawake Zanzibar (ZAFELA) Taasisi ya Pemba Gender Advocacy and Environmental Organization (PEGAO) na Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania, Zanzibar (TAMWA ZNZ) kwa kushirikiana na Ubalozi wa Norway chini Tanzania.

 

Comments

BLOG'S VISITORS

DAKTARI MWENGINE CHAKE CHAKE KULA SIKUKUU POLISI, NI KWA TUHUMA ZA KUMBAKA MGONJWA WAKE

NA WAANDISHI WETU, PEMBA::: DAKTARI anaetoa huduma kwa wagonjwa kituo cha afya cha serikali cha  Gombani wilaya ya Chake Chake Pemba, Is-haka Rashid Hadid, anaendelea kushikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa kaskazini Pemba, akituhumiwa kumtorosha na kisha kumbaka mtoto wa mwenye umri wa miaka 16, mkaazi wa Gombani. Daktari huyo miaka 35 ni mkaazi wa Kangagani Wilaya ya Wete mkoani humo, ambapo anadaiwa alimchukua mtoto huyo kutoka kwa rafiki yake, na kumpeleka kwenye nyumba anayoishi eneo la Kangagani. Mtoto aliefanyiwa kitendo hicho alisema kuwa, April 21 mwaka huu alikwenda kituo cha afya Gombani, kwa ajili ya matibabu na baada ya kupatiwa huduma na daktari huyo, alimuomba nambari yake ya simu. Alisema ilipofika usiku, walikuwa wanawasiliana kupitia ujumbe mfupi (sms) kwa lengo la kwenda kuchukua dawa nyingine ambazo kwa mchana huo alizikosa hospitalini hapo. "Nilikwenda hospitali kutibiwa, baada ya kufanya mapele katika sehemu zangu za siri, lakini akaniambia mpaka aje da

'MKAPA' NA WENZAKE PEMBA WALAZWA RUMANDE

  NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@ MAHKAMA kuu Zanzibar kisiwani Pemba, chini ya Jaji Ibrahim Mzee Ibrahim, imewapeleka rumande watumuhimwa wanne wanaokabiliwa na tuhuma za kuua kwa makusudi, akiwemo Ali Mussa Omar ‘ Mkapa’ mkaazi wa Wawi wilaya ya Chake chake Pemba. Watuhumiwa wengine walioanza maisha mapya ya rumande ni mtuhumiwa Yassir Mohamed Juma miaka 23, Anuwari Mussa Omar miaka 30 pamoja na mtuhumiwa Yassir Mussa Omar ‘ Makababu ’ miaka 29, wote wakaazi wa shehia ya Wawi, wilaya ya Chake chake Pemba. Awali watuhumiwa hao waliwasili mahakamani hapo, kwa mara ya kwanza, kwa ajili ya kusomewa tuhma zinazowakabili za kumuua kwa maksudi Said Seif Kombo. Ilidaiwa mahakamani hapo na Mwendesha Mashtaka kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashataka Seif Mohamed Khamis akiambatana na mwenzake Mussa Khamis Ali kuwa, watuhumiwa hao kwa pamoja wanadaia kufanya mauwaji hayo kwa maksudi. Ilidai kuwa, watuhumiwa wote kwa pamoja, walitenda kosa hilo Oktoba 16, mwaka huu, baina ya saa 7:00 mchan

HII KALI MBUNGE ASIYA AMKOGESHA MWANANCHI HADHARANI KISA HICHI HAPA......

  NA HAJI NASSOR, PEMBA MBUNGE wa viti maalum nafasi za wanawake mkoa wa kaskazini Pemba Asiya Sharif Omar, amewataka wananchi wa kijiji cha taifu, shehia ya Kinyasini jimbo la Gando wilaya ya Wete Pemba, kuyalinda miundombinu ya maji safi na salama, ili yawe endelevu kwao. Kauli hiyo ameitoa wakati alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi, mara baada ya kuwasili kijijini humo, na kumkogesha mwananchi mmoja kama ishara ya uzinduzi wa mradi wa maji safi na salama, ulioasisiwa na mbunge wa Jimbo la Gando. Alisema, hawana mbadala kwa sasa bali ni kuilinda miundombinu ya huduma hiyo, hasa baada ya mbunge wa wao Salim Mussa Omar, kuwarejeshea huduma hiyo. Alieleza kuwa, inafahamika kuwa kwa miaka 14 waliikosa huduma hiyo hasa kwa vile viongozi waliokuwepo hawakujali kuwatatulia tatizo hilo, hadi juzi ilipofanywa na mbunge wao. “Baada ya huduma hii sasa kurejeshwa na mbunge wa jimbo la Gando, kazi iliyobakia kwenu wananchi ni kila mmoja kuwa mlinzi wa miundombinu hii,’’ali

TUHMA ZA DAKTARI PEMBA KUCHIWA HURU: POLISI KASKAZINI KUTOA TAARIFA RASMI LEO

  NA HAJI NASSOR, PEMBA KAMANDA wa Polisi mkoa wa kaskazini Pemba, Juma Saad Khamis, amesema leo Mei 9, mwaka huu atatoa taarifa rasmi, juu ya kuendelea kumshikilia au kumpa dhamana ya Polisi, daktari wa Kituo cha Afya Gombani Is-haka Rashid Hadid, anayetuhumiwa kwa ubakaji. Alisema, kwa vile alikuwa katika mapumziko mafupi, haelewi jambo lolote linaloendelea kwa mtuhumiwa huyo, juu ya kuendelea kushikiliwa kwake kituoni hapo. Alieleza kuwa, leo Mei 6 (jana), hajapata taarifa za ndani za mtuhumiwa, huyo na kuwataka wananchi na wanaharakati, wasubirie hadi Jumatatu ijayo. Akizungumza na waandishi wa habari kwa nyakati tofauti Kamanda huyo, alisema hana taarifa zozote za kupewa dhamana mtuhumiwa ndani ya kituo chake cha Polisi au kuendelea kuwepo. ‘’Ilikuwa mimi sipo kazini kwa muda, kuanzia anakamatwa hadi anafikishwa Polisi, kwa sasa siwezi kueleza jambo lolote kwa mtuhumiwa huyo, hadi Jumatatu,’’alieleza. Aidha Kamanda huyo alieleza kuwa, kwa sasa hawezi kutoa ufafan

MADAKTARI KUTOKA CHINA WAOKOA MAISHA YA MTOTO PEMBA

  HABIBA ZARALI, PEMBA TIMU ya 32 ya madaktari wa kichina katika hospitali ya Abdalla Mzee Mkoani wamefanikiwa kufanya upasuaji mkubwa wa mtoto mwenye umri wa miaka 15 mkaazi wa Chole Kengeja, baada ya kuchomwa na jiti sehemu ya njia zake za mfumo wa uzazi. Mtoto huyo ambae alianguka hivi karibuni katika mti na baadae kuchomwa na jiti hilo na kumsababishia kutokwa na damu nyingi katika sehemu ya nyonga, alifanyiwa upasuaji uliodumu kwa muda wa saa tatu na   kuokolewa maisha yake. Akizungumza mara baada ya operesheni huo kiongozi wa timu hiyo Dr Jiang Jinhua, alisema mara baada ya mtoto huyo kufikishwa hospitalini hapo na kufanyiwa vipimo na kuonekana   ilibidi apatiwe rufaa ya kwenda katika hospitali nzuri yenye kutibu tatizo lake huko nchini Kuwado ambapo haikuwezekana kutokana na hali ya umaskini wa f amilia ya mtoto huyo . Alisema timu ya madaktari hao itaendelea kutowa huduma za matibabu   kwa wananchi kisiwani humo,   ili kuwaondolea gharama ya kutafuta matibabu nje ya nch