Skip to main content

UNYANYAPAA TISHIO JIPYA VIPAJI VYA WATOTO WA KIKE WENYE UALBINO

 


NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@

‘MICHEZO kwa wote ‘or sport for all’’.

Michezo kwa maendeleo endelevu, michezo ni ajira, afya, udugu na kujenga uhusiano wa kudumu.

Wapo walioinadi kuwa, michezo ni sehemu ya maisha ya mwanadamu yeyote yule, bila ya kujali rangi, kabila wala jinsia.

Kwa mfano sheria 17 za mpira wa miguu, hazijambagua mtu yeyote, chamsingi awe anajimudu kufikia miundombinu husika.

Miongoni mwa vifungu vya sheria hiyo, ili kandanda ifanyike moja ni uwepo wa uwanja, pili ni mpira, idadi ya wachezaji, vifaa vya michezo, mwamuzi pamoja na sheria ya 17 ya pigo la kona.

Wapo wanawake warefu, wafupi, wanene, wembamba na hata kwa wanaaume, wapo katika maeneo kama hayo, wakishiriki michezo mbali mbali.

Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984, kwenye sura yake ya tatu na hasa kifungu cha 11, kimebainisha usawa wa binaadamu.

Hata kile cha 12, kikaendelea kuweka usawa mbele ya sheria, cha 13 haki ya kila mmoja kuwa hai, 14 haki ya uhuru wa mtu binafsi pamoja na kila cha 18 cha haki ya kutoa maoni.

Mkataba wa kimataifa wa haki za watu wenye ulemavu, ibara ya 5 imekataza ubaguzi, ukisema watu wote ni sawa mbele ya sheria.

Kubwa zaidi mkataba huu, ibara ya 30, ukachambua haki ya kushiriki katika utamaduni, burudani na michezo kwa watu wenye ulemavu.

Ukaenda mbali zaidi, ukisema lazima nchi zilizoridhia mkataba huu Tanzania ikiwemo, ‘kuhakikisha watu wenye ulemavu, wanafurahia upatikanaji vifaa vya michezo’.

Kifungu 30 (b) kikaeleza jingine, ambalo ni haki watu wenye ulemavu kuhakikisha wanajengewa uwezo wa kushiriki michezo, na (e) watoto wenye ulemavu wanapata haki sawa kushiriki michezo kadhaa.

Kumbe hata sheria ya watu wenye ulemavu Zanzibar nambari 8 ya mwaka 2022, kifungu cha 28 (1), (f) kimesisitiza haki moja wapo kwao, ni kushiriki michezo na burudani.

Sheikh Said Ahmad Mohamed wa Chake chake, anasema Qur-an haijambagua mtu kwa sababu ya ulemavu wake, ngozi, jinsia wala eneo analotoka.



‘’Umeweka wazi dhana ya mtoto wa kike wa kiislamu, kushiriki michezo, na hasa ikiwa kwa umri wake ameshakuwa mtu mzima, moja ni kivazi na kutojichanganya na wanaume,’’anasema.

Kumbe dini, mikataba, sheria, kanuni, katiba na maazimio yote ya ulimwenguni, hayajambagua mtoto wa kike mwenye ualbino, kushiriki michezo.

WAZAZI WA WATOTO WENYE UALBINO WANASEMAJE

Omar Hassan Omar (58) wa Wawi mwenye mtoto wa kike mwenye ualbino, anasema mtoto wake alianza unyanyapaa akiwa skuli, na kushindwa kushiri hata mchezo mmoja.

Anasema, alikuwa akisoma skuli ya Bububu kisiwani Unguja, ingawa mwaka 2019, aliamua kuhama nae kumleta kisiwani Pemba.

‘’Alikuwa mzuri kwenye mchezo wa kuruka chini ‘long jump’ ingawa wenzake walimpa majina mabaya mingi, na kujiskia mnyonge,’’anasema.

Mama mzazi wa mtoto huyo, Aisha Mwadini Ali, anasema hata kwenye utunzi wa mashairi, alitokea mshindi wa kwanza wa kitaifa.

‘’Alipewa majina mabaya ambayo sipendi kuyatamka, na kisha yalimkatisha tamaa kuendelea na masomo,’’anafafanua.


Ameir Haji Omar (40) mkaazi wa Mkanjuni Chake chake, anasema, watoto wa kike wenye ualbino, wanauwezo mkubwa wa kushiriki michezo, ingawa unyanyapaa unadidimizi vipaji vyao.

‘’Mimi nilikuwa nasomesha skuli moja ya binafsi hapa Pemba, lakini hata waalimu wenzangu hawakuwa wakimpa kipaumbele watoto wa aina hii,’’anafafanua.

Maryam Himid Khalfan ‘anti mamu’ wa Mtambile anasema mtoto wa kike wa jirani yake, ameshindwa hata kusafiri na wenzake, kushiriki sherehe za elimu bila malipo Unguja.

‘’Ni mwanafunzi alikuwa mshindi wa mbio za mita 100, kimkoa, lakini kutokana na unyanyapaa kwa wenzake, aliamua nafasi yake kumpa mshindi wa pili asafiri,’’anahadithia.

Kaka wa kambo wa mtoto huyo Omar Ussi Hamad, anasema watoto wa kike, bado wanakabiliwa na unyanyapaa wa kubandikwa majina mabaya kwa aina walivyo.

‘’Mdogo wangu alikuwa muwekezaji mzuri kwenye mbio fupi, lakini alikuwa anapewa majina mabaya, na kukatisha ndoto zake,’’anasema.

WAATHIRIKA

Mtoto huyo anasema, bado hawajatendewa haki na jamii iliyokubwa, kwa kule kumpa majina nayoyakataa na kimsingi hayako kwenye ubinaadamu.

Anasema, wakati anasoma darasa la tisa, hakuwahi kushika nambari ya pili, kwenye mbio za mita 100, daima alikuw amshindi, ingawa alikuwa anakabiliwa na unyanyapaa.

‘’Sio kama hatuna uwezo wa kushiriki michezo kama riadha, kuogolea, Sanaa, lakini jamii tena iliyotuzunguruka wanatunyanyapaa kwa kutubandika majina ya hovyo,’’anasema.

Hamida Issa Mjaka (17) mwenye ualibino mkaazi wa Michekaini Chake chake, anasema aliwahi mara moja akiwa darasa la nne, kushirki michezo na alishinda.

‘’Eti yule niliyemshindwa anachekwa, kwamba unapitwa na hata mwenye ualbino, sasa nikisikia hivyo, huwa napata aibu,’’anasema.

Mayasa Ibrahim Hamad wa Wesha, anasema wao wamekuwa hawashirikishwi, kushiriki michezo kutokana na ulemavu wao walionao.

‘’Watu wanapenda kutupa majina tunayoyachukia, hivyo hata pakianzishwa timu za wilaya, mkoa, taifa hutuingizwi na tukiingizwa tunakosa amani,’’analalamika.

Mtumwa Khamis Nassor, anasema mwaka 2022, alitamani kuingia kwenye mpira wa mikono, ingawa wachezaji wenzake wanawake hawakuwa wakimpa nafasi.

JAMII INAMTAZAMO GANI?

Omar Khamis Omar wa Kengeja, anasema ni vigumu wao kushiriki michezo, kutokana na hali zao, hasa kwa ile inayotumia nguvu.

‘’Mimi sioni umuhimu wa wao kushiriki michezo, maana ipo mingine inatumia nguvu na wao wanashida ya ngozi, sasa labda wawe peke yao,’’anafikiria.

Aisha Said Khalfan wa Mtambile, anasema kama jamii itawakubali na kuwapa nafasi, wanaweza kufanya vizuri watoto wa kike, wenye ualbino hadi kimataifa.

‘’Tunaona kwa wenzetu ambao wanawaamini, wanashiriki michezo mbali mbali na wanafanya vizuri,’’anasema.

Mohamed Mzale Mjaka wa Mwambe Mkoani, anasema watoto wa kike wenye ualbino, ni sawa na wengine, ikiwa familia zao zitaamua kuekeza kwao,’’anasema.

Mwanamichezo mkongwe kisiwani Pemba Asha Nassor Sultan [TOP] wa Chake chake, anasema hakuna uhusiano kati ya ualbino na michezo.

‘’Suala la michezo ni kwa jamii zote, wawe watu wenye ulemavu, wafupi na wingine, kubwa zaidi ni jamii kuondoa unyanyapaa,’’anasema.

Maana anasema, kwao kuna unyanyapaa uliokithiri ikiwemo kupewa majina mabaya, na wakiwa wakubwa wanaweza kuitwa wahuni.

Anaona bado suala la michezo kwa watoto wa kike, linachukuliwa kinyume mbele na jamii, na kuvifanya vipaji vyao kufifia.

Mashavu Juma Mabrouk wa Baraza la taifa la watu wenye Ulemavu Zanzibar, anasema kama jamii itaendelea na mtazamo mbaya, watoto hao wanaweza kufa na vipaji vyao.

‘’Tunaendelea kuelimisha, lakini bado watoto wa kike wenye ualbino, hawajaaminiwa kwenye kushiriki michezo, kuanzia skuli, mitaani hadi timu za wilaya,’’anasema.

TAMWA ZANZIBAR INAFANYAJE?

Afisa Mradi wa kukuza usawa wa kijinsia na ujumuishi kwenye michezo, Khairat Haji anasema Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania-TAMWA- Zanzibar, wameona ipo haja ya kushirikiana na vyombo vya habari, kuibua changamoto za aina hiyo.



Kiujumla watoto wa kike na hasa wenye ulemavu tena wa ualbino, wamezungurukwa na darzeni ya changamoto, zinazowarejesha nyuma kushiriki michezo.

Kumbe kabla ya kuwa mradi huo, walifanya utafiti mdogo, ambao waligundua kuwa, kuna mifumo dume na yale mawazo mgando, ambayo ni vikwazo dhidi ya wanawake na watoto wa kike kushiriki michezo.

Kupitia mradi wa michezo kwa maendeleo, unaodhaminiwa na shirika la Maendeleo la Kimataifa la Ujerumani (GIZ) wanakusudia, kila mmoja aweze kushiriki michezo.

Mradi huo kwa sasa, unatekelezwa na Jumuiya ya wanasheria wanawake Zanzibar ‘ZAFELA’ Kituo cha mijadiliano kwa vijana ‘CYD’ pamoja na TAMWA-Zanzibar kwa ufadhili Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Ujerumani ‘GIZ’

Lengo ni kuongeza ushiriki wa wanawake na watoto wa kike, katika mazoezi na michezo, kwani kila mtu, anayo haki sawa, katika eneo hilo.

‘’Jukumu letu ni kuwawezesha waandishi wa habari kimafunzo, na kisha wawe weledi wa kukuza usawa wa kijinsia na ujumuishi, katika michezo, kupitia kazi zao,’’anaeleza.

Kwa sasa tayari waandishi 30 wa Zanzibar, wameshawezeshwa namna bora ya kuandika habari na kutengeneza vipindi, vinavyoelezea fursa sawa ya michezo na eneo la ujumuishi.

Kuhusu changamoto, anasema zilizoibuliwa, ni kuinasibisha michezo na mazoezi kwa mtoto wa kike na wanawake, ni uhuni, jambo ambalo sio sahihi.

UPI MCHANGO WA WIZARA HUSIKA KATIKA HILI

Kaimu Mratibu Idara ya Utamaduni na Michezo Pemba, Khamis Hamad Juma, anasema haijawahi kutokeza kuwepo kwa mashindano maalum ya mchezo wa aina yoyote, kwa watoto wa kike wenye ulemavu.

 ’Hata bonanza la michezo, ambalo ni maalum kwa ajili ya watoto wa kike wenye ulemavu, sijawahi kuliona wala kusikia,’’anafafanua.

Hapa Waziri wa Habari Tabia Maulid Mwita, anasema moja ya mchango wa wizara katika kuinua michezo kwa watu wenye ulemavu, baraza la michezo liliwa kuvisaidia vyama vitatu (3) vya michezo ya watu wenye ulemavu, katika kuandaa na kushiriki mashindano kadhaa.

Moja na mashindano hayo yakiwemo kitaifa ya michezo ya watu wenye ulemavu wa akili, yaliyofanyika mwaka 2022.

Hayo yamefahamika wakati Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo Tabia Maulid Mwita, akisoma bajeti ya mwaka wa fedha 2022/2023.

 Akasema Zanzibar, ilifanikiwa kupata medali 20 zikiwemo dhahabu nane, fedha moja, na shaba 11, katika michezo tofauti, kupitia timu za watu wetu wenye ulemavu wa akili.

Kwenye michezo ya watu wenye ulemavu wa mguu na mkono mmoja, wizara imelisaidia shirikisho la mchezo huo, na kushiriki mashindano ya kitaifa yaliyofanyika Arusha.

 Lakini shirikisho la michezo ya viziwi Zanzibar (SHIMIVIZA), limesaidiwa kuandaa bonanza kwa ajili ya kuadhimisha siku ya viziwi duniani.

 

                Mwisho

Comments