Skip to main content

UBAKAJI WA WATOTO, UNAVYOKIWEKA KISIWA CHA PEMBA SHAKANI

 



NA ZUHURA JUMA, PEMBA@@@@

VIONGOZI, wanaharakati na wataalamu wa masuala ya saikolojia wameonya kuhusu athari za muda mrefu zitakazotokea kisiwani Pemba na Zanzibar kwa ujumla, endapo vitendo vya ubakaji vitaachwa bila kuchukuliwa hatua.

Katika miaka ya karibuni, kumekuwa na matukio mengi ya mabinti ambao hawajafikia umri wa kuruhusiwa kushiriki ngono kubakwa, lakini wahusika kuachiwa baada ya kesi kuondolewa mahakamani.

Katika mahojiano yaliyofanywa kati ya mwandishi wetu na makundi tofauti, ilielezwa kwamba hali hii ya sasa kama itaendelea, kuna hatari ya jamii ya Pemba kupata athari za muda mrefu.

Moja iliyotajwa ni wingi wa watoto wasio na familia, waathiri wa ubakaji wenye msongo wa mawazo na kujengeka kwa utamaduni wa watu kutotii sheria.

Mkaazi wa Shehia ya Minungwini, Maulid Saleh Hamad, anasema hofu yake kubwa, ni kwamba kuna athari nyingi zitajitokeza ikiwa ni pamoja na wabakaji kuzidi kusambaa kwenye mitaa yao na kupata nguvu zaidi ya kudhalilisha watoto.

Bakari Suleiman Juma wa Shehia ya Kambini anasema wana hofu kubwa kwamba vitendo hivyo vitakuwa endelevu na pia watoto wataendelea kufanyiwa ubakaji kila siku kwa vile wale wanaomdhalilisha hawapati hukumu yeyote.

“Mtoto anapofanyiwa udhalilishaji ni vigumu kutimiza malengo yake aliyoyakusudia kwani walio wengi hawarudi tena skuli kusoma”, anaeleza.

Mkaazi mwingine wa Shehia ya Mitondooni Kambini, Riziki Abdallah anaeleza kuwa, mtoto anayekataa kutoa ushahidi ataendelea kudhalilishwa na watoto wengine watakuwa wanashawishiana kuendelea na vitendo hivyo.

“Aghalabu wanapokwenda hurubuniwa kwa pesa, hivyo anapoona nikienda kwa fulani ananipa pesa, anamwambia na mwenzake na mwisho wa siku ni kuambukizana mchezo mchafu”, anasema.

Mwanaharakati Siti Faki Ali anasema, watoto wataathirika kisaikolojia na kimaumbile kwa sababu kuna kesi nyingi ambazo daktari huthibitisha tayari ameshaharibika fuko la uzazi au haja ndogo na kuharibika sehemu za siri.

“Kwa hali hiyo, inawezekana huko mbele kukosa kizazi kwa sababu tayari ameshakuwa mbovu na hivyo taifa kukosa nguvu kazi”, anaeleza mwanaharakati huyo.

Khadija Hassan Ali mkaazi wa Piki anaeleza kuwa athari ni kubwa kwani, waathirika wa vitendo vya ubakaji huathirika kiakili, wengine hukosa kizazi na pia huwa watu wenye kuona aibu bila sababu katika maisha yao yote.

Hakimu wa Mahakama Maalumu ya kushughulikia kesi za Udhalilishaji Mkoa iliyopo Wete, Ali Abdulrahman Ali, anataja athari kubwa ya kuachia washitakiwa ni kuwa haki inashindwa kupatikana.

“Kesi za ubakaji zilizofikishwa mahakamani mwaka 2020 ni tisa (9), kati ya hizo watoto wenye miaka 15-17 ni kesi tatu ingawa moja tu ndio iliyopata hatia na mbili ziliondoshwa”, anafafanua.

Afisa Ustawi wa Jamii Pemba, Omar Mohamed, anaeleza kuwa athari kubwa inayoweza kutokea ni kuongezeka kwa vitendo hivyo vya ubakaji hasa pale wahalifu watakapoona hatua hazichukuliwi kwa vitendo vyao.

‘’Vilevile watoto wataendelea kudhalilishwa na hatimaye kuambukizwa maradhi mbali mbali, ikiwemo ukimwi na mwisho wa siku watashindwa kutimiza ndoto zao za kimaisha walizokuwa nazo kwa muda mrefu,’’anaeleza.

Mratibu wa Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA) Pemba, Fat-hiya Mussa Said, anasema athari ni kutokuwepo kwa kesi itakayopata hatia kwa sababu kesi yeyote haiwezi kupata hukumu bila ya kutolewa ushahidi mahakamani.



‘’Tena unatakiwa ushahidi usio na shaka, hivyo ikiwa ushahidi hakuna, kila siku matukio yatazidi kwa sababu washtakiwa itakuwa hawapati kutiwa hatiani’’, anaeleza.

Baba mmoja ambaye hakutaka jina lake litajwe mkaazi wa Kiuongoni anakumbuka kuwa, kuna kesi ilitokea kijijini kwao hivi karibuni, ambapo familia zote mbili walikubaliana mtoto aharibu ushahidi, ili wazazi wake wapewe shilingi milioni mbili.

“Na kweli mtoto huyo mwenye miaka 15 alibadilisha ushahidi na ilikuwa kila wanapoitwa hawataki kwenda mahakamani, hatimae kesi ilifungwa, kilichowafanya wajutie sasa, baada ya mtuhumiwa kutoka mpaka leo hawajapewa pesa”, anasimulia.

Anasema kwamba, sasa familia hiyo imebaki kulalamika na kusema wataenda tena kuifungua kesi hiyo, jambo ambalo linamshangaza sana kwani chungu ni moto wa mwanzo wahenga walisema.

“Hiyo ndio athari kwa sababu mtoto wao ameshabakwa, baadaye wakamshawishi asiseme ukweli, hivyo sasa yupo ameshakosa haki yake huku mwanamme akidunda mitaani”, anaelezea.

Sheikh Mussa Saleh Ali anasema, athari zinazoweza kutokea iwapo watoto hao wataendelea kukataa kutoa ushahidi, ni kwamba aliyefanya kitendo hatopata kuhukumiwa, kwani ushahidi itakuwa umepotea.

Taarifa za kimahakama zinaonyesha kuwa kuanzia mwaka 2020 hadi 2021, jumla ya kesi zinazohusu ubakaji wa mabinti wadogo zilikuwa ni 49 huku za watoto kati ya umri wa miaka 15-17 zikiwa 19. Katika kesi hizo, kesi ambazo wahusika wamefungwa ni nne tu huku mbili wahusika wakitozwa faini na nyingine 13 zikiwa zimeondolewa mahakamani.

Pia, takwimu hizo zinaonyesha kwamba kwa mwaka 2021, kesi za kubaka zilizofikishwa mahakamani ni 25, huku zinazohusu watoto wenye miaka 15-17 ni 16, ambapo kesi 11 zimeondolewa, kesi tatu washtakiwa wamefungwa na kesi mbili washtakiwa wametozwa faini kutokana na kuwa wapo chini ya miaka 18.

Uchunguzi wa mwandishi kuhusu suala hili umebaini kwamba moja wapo ya sababu zinazosababisha kesi za ubakaji kuishia namna hii ni ukweli kwamba wahusika huwa wanajuana kwa ama kuwa jirani, familia moja au ndugu wa karibu.

Kumekuwa na kesi nyingi ambazo hufutwa kituo cha Polisi na mahakamani kwa kukosa ushahidi, hasa zile za watoto wenye umri kuanzia miaka 15 hadi 17, jambo ambalo linaleta athari mbalimbali kwa familia, jamii, taifa na mtoto mwenyewe.

Pamoja na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) kuweka mikakati itakayosaidia kesi hizo kusikilizwa kwa haraka na kupatiwa hukumu kwa lengo la kutokomeza vitendo hivyo, lakini bado kesi za watoto wenye umri huo zinaendelea kufutwa.

                                            Mwisho

                                                      

 

 

 

   

Comments

BLOG'S VISITORS

DAKTARI MWENGINE CHAKE CHAKE KULA SIKUKUU POLISI, NI KWA TUHUMA ZA KUMBAKA MGONJWA WAKE

NA WAANDISHI WETU, PEMBA::: DAKTARI anaetoa huduma kwa wagonjwa kituo cha afya cha serikali cha  Gombani wilaya ya Chake Chake Pemba, Is-haka Rashid Hadid, anaendelea kushikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa kaskazini Pemba, akituhumiwa kumtorosha na kisha kumbaka mtoto wa mwenye umri wa miaka 16, mkaazi wa Gombani. Daktari huyo miaka 35 ni mkaazi wa Kangagani Wilaya ya Wete mkoani humo, ambapo anadaiwa alimchukua mtoto huyo kutoka kwa rafiki yake, na kumpeleka kwenye nyumba anayoishi eneo la Kangagani. Mtoto aliefanyiwa kitendo hicho alisema kuwa, April 21 mwaka huu alikwenda kituo cha afya Gombani, kwa ajili ya matibabu na baada ya kupatiwa huduma na daktari huyo, alimuomba nambari yake ya simu. Alisema ilipofika usiku, walikuwa wanawasiliana kupitia ujumbe mfupi (sms) kwa lengo la kwenda kuchukua dawa nyingine ambazo kwa mchana huo alizikosa hospitalini hapo. "Nilikwenda hospitali kutibiwa, baada ya kufanya mapele katika sehemu zangu za siri, lakini akaniambia mpaka aje da

'MKAPA' NA WENZAKE PEMBA WALAZWA RUMANDE

  NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@ MAHKAMA kuu Zanzibar kisiwani Pemba, chini ya Jaji Ibrahim Mzee Ibrahim, imewapeleka rumande watumuhimwa wanne wanaokabiliwa na tuhuma za kuua kwa makusudi, akiwemo Ali Mussa Omar ‘ Mkapa’ mkaazi wa Wawi wilaya ya Chake chake Pemba. Watuhumiwa wengine walioanza maisha mapya ya rumande ni mtuhumiwa Yassir Mohamed Juma miaka 23, Anuwari Mussa Omar miaka 30 pamoja na mtuhumiwa Yassir Mussa Omar ‘ Makababu ’ miaka 29, wote wakaazi wa shehia ya Wawi, wilaya ya Chake chake Pemba. Awali watuhumiwa hao waliwasili mahakamani hapo, kwa mara ya kwanza, kwa ajili ya kusomewa tuhma zinazowakabili za kumuua kwa maksudi Said Seif Kombo. Ilidaiwa mahakamani hapo na Mwendesha Mashtaka kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashataka Seif Mohamed Khamis akiambatana na mwenzake Mussa Khamis Ali kuwa, watuhumiwa hao kwa pamoja wanadaia kufanya mauwaji hayo kwa maksudi. Ilidai kuwa, watuhumiwa wote kwa pamoja, walitenda kosa hilo Oktoba 16, mwaka huu, baina ya saa 7:00 mchan

HII KALI MBUNGE ASIYA AMKOGESHA MWANANCHI HADHARANI KISA HICHI HAPA......

  NA HAJI NASSOR, PEMBA MBUNGE wa viti maalum nafasi za wanawake mkoa wa kaskazini Pemba Asiya Sharif Omar, amewataka wananchi wa kijiji cha taifu, shehia ya Kinyasini jimbo la Gando wilaya ya Wete Pemba, kuyalinda miundombinu ya maji safi na salama, ili yawe endelevu kwao. Kauli hiyo ameitoa wakati alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi, mara baada ya kuwasili kijijini humo, na kumkogesha mwananchi mmoja kama ishara ya uzinduzi wa mradi wa maji safi na salama, ulioasisiwa na mbunge wa Jimbo la Gando. Alisema, hawana mbadala kwa sasa bali ni kuilinda miundombinu ya huduma hiyo, hasa baada ya mbunge wa wao Salim Mussa Omar, kuwarejeshea huduma hiyo. Alieleza kuwa, inafahamika kuwa kwa miaka 14 waliikosa huduma hiyo hasa kwa vile viongozi waliokuwepo hawakujali kuwatatulia tatizo hilo, hadi juzi ilipofanywa na mbunge wao. “Baada ya huduma hii sasa kurejeshwa na mbunge wa jimbo la Gando, kazi iliyobakia kwenu wananchi ni kila mmoja kuwa mlinzi wa miundombinu hii,’’ali

TUHMA ZA DAKTARI PEMBA KUCHIWA HURU: POLISI KASKAZINI KUTOA TAARIFA RASMI LEO

  NA HAJI NASSOR, PEMBA KAMANDA wa Polisi mkoa wa kaskazini Pemba, Juma Saad Khamis, amesema leo Mei 9, mwaka huu atatoa taarifa rasmi, juu ya kuendelea kumshikilia au kumpa dhamana ya Polisi, daktari wa Kituo cha Afya Gombani Is-haka Rashid Hadid, anayetuhumiwa kwa ubakaji. Alisema, kwa vile alikuwa katika mapumziko mafupi, haelewi jambo lolote linaloendelea kwa mtuhumiwa huyo, juu ya kuendelea kushikiliwa kwake kituoni hapo. Alieleza kuwa, leo Mei 6 (jana), hajapata taarifa za ndani za mtuhumiwa, huyo na kuwataka wananchi na wanaharakati, wasubirie hadi Jumatatu ijayo. Akizungumza na waandishi wa habari kwa nyakati tofauti Kamanda huyo, alisema hana taarifa zozote za kupewa dhamana mtuhumiwa ndani ya kituo chake cha Polisi au kuendelea kuwepo. ‘’Ilikuwa mimi sipo kazini kwa muda, kuanzia anakamatwa hadi anafikishwa Polisi, kwa sasa siwezi kueleza jambo lolote kwa mtuhumiwa huyo, hadi Jumatatu,’’alieleza. Aidha Kamanda huyo alieleza kuwa, kwa sasa hawezi kutoa ufafan

MADAKTARI KUTOKA CHINA WAOKOA MAISHA YA MTOTO PEMBA

  HABIBA ZARALI, PEMBA TIMU ya 32 ya madaktari wa kichina katika hospitali ya Abdalla Mzee Mkoani wamefanikiwa kufanya upasuaji mkubwa wa mtoto mwenye umri wa miaka 15 mkaazi wa Chole Kengeja, baada ya kuchomwa na jiti sehemu ya njia zake za mfumo wa uzazi. Mtoto huyo ambae alianguka hivi karibuni katika mti na baadae kuchomwa na jiti hilo na kumsababishia kutokwa na damu nyingi katika sehemu ya nyonga, alifanyiwa upasuaji uliodumu kwa muda wa saa tatu na   kuokolewa maisha yake. Akizungumza mara baada ya operesheni huo kiongozi wa timu hiyo Dr Jiang Jinhua, alisema mara baada ya mtoto huyo kufikishwa hospitalini hapo na kufanyiwa vipimo na kuonekana   ilibidi apatiwe rufaa ya kwenda katika hospitali nzuri yenye kutibu tatizo lake huko nchini Kuwado ambapo haikuwezekana kutokana na hali ya umaskini wa f amilia ya mtoto huyo . Alisema timu ya madaktari hao itaendelea kutowa huduma za matibabu   kwa wananchi kisiwani humo,   ili kuwaondolea gharama ya kutafuta matibabu nje ya nch