Skip to main content

WADAU WA HABARI ZANZIBAR WATAKA SHERIA ISIYOUMIZA

 






  

                           


NA SALUM VUAI, ZANZIBAR;

KWA miaka mingi sasa, sekta ya habari visiwani Zanzibar, licha ya kupata mafanikio kadhaa, lakini imekuwa ikikabiliwa na changamoto mbalimbali zinazobana uhuru wa waandishi kutoa na wananchi kupata habari.

 

Ingawa uhuru umeongezeka kwa kiasi fulani, lakini bado baadhi ya watu wamejenga dhana kwamba waandishi wa habari ni maadui wanaopasa kuogopwa kama nyoka mwenye sum kali.

 


Mara kwa mara, waandishi wa vyombo vya habari ama wameripoti kunyimwa taarifa au kuamriwa kutozitangaza hasa pale kunapokuwa na matukio yanayoshtua umma ambayo yana chembechembe za uzembe wa viongozi na watendaji wakuu wa serikali.

 

Hali inakuwa mbaya zaidi pale ambapo hata viongozi wa serikali na taasisi zake wanapokataa kutoa ushirikiano kwa waandishi endapo watabaini wanatafuta ukweli juu ya taarifa zinazogusa maslahi yao binafsi.

 

Hata hivyo, viongozi kama hao wanakuwa marafiki wakubwa kwa waandishi wanapotaka kutangazwa vizuri na kusifiwa kwa mambo wanayodhani yanaweza kuwajenga.

Ili kuondoa vikwazo hivyo, marekebisho ya sheria ya habari kimekuwa kilio kikubwa kwa waandishi, wakidai sheria mpya inayokwenda na wakati uliopo na isiyokuwa na masharti yanayoumiza.

Ifahamike kuwa, uhuru wa habari na kutoa maoni, ni miongoni mwa haki za binadamu zilizomo katika mikataba mbalimbali ya kitaifa na kimataifa.

 

Hiyo inatokana na masuala ya haki hizo za binadamu kuanza kuingizwa katika mikataba hiyo mnamo mwaka 1950 baada ya dunia kuweka Azimio la kuzilinda kimataifa (Universal Declaration of Human Rights-UDHR) lililofikiwa mwaka 1948.

 

Kama hiyo haitoshi, barani Afrika, suala la haki za binadamu liliainishwa katika mkataba wa Afrika kuhusiana na jambo hilo lililopitishwa mwaka 1981.

 

Mwandishi wa makala haya pamoja na kupekua nyaraka tofauti zinazozungumzia haki ya kutoa na kupata maoni, pia alizungumza na baadhi ya waandishi wa habari wakongwe sambamba na wanaharakari kadhaa ambao ni wadau wa habari.

 

Mazungumzo hayo yalijielekeza katika umuhimu wa kutaka kuharakishwa kwa sheria mpya ya habari itakayokata minyororo inayokwaza upatikanaji wa habari nchini, lakini pia isiyotafuna.

 

Mwenyekiti wa Jumuia ya Waandishi wa Habari za Maendeleo Zanzibar Hawra Shamte, akitoa mada katika warsha ya kuchechemua waandishi juu ya sheria mpya ya habari iliyofanyika Juni 25, 2022 ukumbi wa sanaa Rahaleo, alikuwa na haya ya kusema:

 

“Haki ya uhuru wa kujieleza ambayo pia inahusu haki ya uhuru wa habari inalindwa  chini ya Ibara ya 18 ya Katiba ya Zanzibar,” alisema.

 

Ibara hiyo 18 (1) inasema: “Bila ya kuathiri sheria nyengine za nchi, kila mtu anayo haki ya uhuru wa maoni (kujieleza), kutafuta, kupokea na kusambaza habari na mawazo yake kupitia chombo chochote cha habari bila kujali mipaka ya nchi na pia anayo haki na uhuru wa kutoingiliwa mawasiliano yake.

Ibara hiyo hiyo kifungu namba 2, kinasema:

“Kila raia anayo haki ya kupewa taarifa wakati wote wa matukio mbalimbali nchini na duniani kwa jumla ambayo ni muhimu kwa maisha na shughuli za wananchi na pia masuala yenye umuhimu kwa jamii.

 

Hata hivyo, kwa mujibu wa Shamte, akinukuu mapungufu yaliyomo kifungu cha kwanza kama yalivyooneshwa katika rasimu ya marekebisho pendekezwa ya sheria ya habari, kinanyang’anya haki na hivyo kifungu hicho kina makucha.

 

Hapo ilipoelezwa katika kifungu hicho cha Katiba, maneno; “Bila kuathiri sheria nyengine yoyote ya nchi”, kinamaanisha kuwa, kufurahia uhuru wa kujieleza, kutafuta, kusambaza habari, unategemea sheria nyengine za nchi.

Aidha Ibara ya 24 ya Katiba ya Zanzibar imeweka mipaka ya jumla ya haki na uhuru ambayo inasomeka kama ifuatavyo:

 


“Haki za binadamu na uhuru, kanuni zake ambazo zimeainishwa katika Katiba hii, hazitatekelezwa na mtu kwa namna ambayo itasababisha kuingiliwa au kukandamiza haki na uhuru wa watu wengine au maslahi ya umma.”

 

Aya iliyotajwa hapo juu, inaweka bayana kwamba  haki na uhuru huo unaweza kuwekewa mipaka na sheria iliyotungwa na Baraza la Wawakilishi  ikiwa KIZUIZI HICHO NI CHA LAZIMA na kinakubalika katika mfumo wa kidemokrasia.

 

Katika nukuu hizohizo, Shamte alionesha wasiwasi kuwa kifungu hicho kinatoa nafasi kwa Baraza la Wawakilishi kuweka mipaka ya kufurahia uhuru wowote ikiwa ni pamoja na ule wa kujieleza.

 

Kwa maoni hayo na mengine mbalimbali kuhusu uhitaji wa sheria mpya ya habari hapa Zanzibar, uko ulazima Katiba hiyo pia ifanyiwe marekebisho ya haraka na ni wajibu wa waandishi wa habari kuchagiza  jambo hilo lifanyike sasa bila ya ajizi.

 

Haja ya uharaka huo inakuja kwa vile zipo sheria nyengine nyingi zinazoathiri uhuru wa habari na haki ya kujieleza, kwa mfano sheria za usalama wa Taifa, Baraza la Wawakilishi, Takwimu na ile ya makosa ya mtandaoni ambayo imetungwa Tanzania Bara na haijaridhiwa Zanzibar lakini inatumika.

 

Pamoja na mapungufu mengi yaliyomo kwenye sheria ya habari Zanzibar, takriban wadau wote niliotaka maoni yao, wameshauri kuwepo maeneo yanayokataza matumizi makubwa ya nguvu kwa wanahabari pale wanapozuiwa kutafuta taarifa, kupiga picha na baada ya kuzitangaza habari ambazo zitahisiwa kwenda kinyume na sheria za nchi, au japo kwa upande mmoja kutopendezewa tu kutolewa kwa taarifa husika.

 

Wengine walikwenda mbali kwa kusema wakati sasa umefika kuongeza maradufu uhuru wa habari na kujieleza kwa kukopia mfumo wa ‘Hyde Park’ unaotumika nchini Uingereza.

 

Hyde Park ni eneo mashuhuri lililoko Westminster katikati ya London lililoanza karne nyingi nyuma ambalo watu wako huru kukutana na kujadili siasa na mambo mengine ya kijamii yanayohusu jamii zao.

 

Kwa jina maarufu, eneo hilo hujulikana kama ‘Kona ya Spika’ na zamani Polisi walikuwa wakiwazuia watu kwa kuwatoa nje, hadi ilipoamuliwa kuundiwa nafasi ili kuwapa watu uhuru kujadili mambo wayatakayo kwa amani.

 

Kila Jumapili watu husimama juu ya sanduku maalumu na kutoa maoni yao kwa uhuru juu ya siasa, dini au chochote.

 

Inasemekana kuwa sababu ya watu kutakiwa wasimame juu ya sanduku, yatokana na sharti kwamba haipaswi mtu kuikosoa serikali ya Uingereza huku akiwa amekanyaga ardhi ya nchi hiyo.

Kauthar Is-hak ni Ofisa Habari na mwandishi mwandamizi katika Idara ya Habari Maelezo Zanzibar.

 

Alisema dunia ya sasa ni tofauti naya kale ambapo teknolojia imetawala na ndiyo inayowaleta watu pamoja kwa muda mfupi na kwa haraka zaidi.

 


Alieleza kuwa mitandao ya kijamii imerahisisha mawasiliano na hakuna kitu kinachoweza kufichwa.

 

“Huu si wakati wa kufungana midomo, ni kweli uhuru una mipaka lakini ni vigumu kuwadhibiti watu wasitoe joto lao. Muhimu sheria zisiwabane watu kwa kuwa tu kundi la wateule fulani hawataki mambo yajulikane,” alifafanua.

 

Kauthar alikosoa mtindo wa baadhi ya viongozi na watu wengine wenye nyadhifa kubwa, kuwaelekeza waandishi wa habari juu ya mambo ya kuandika na kutangaza, akisema kufanya hivyo ni woga na kutojiamini juu ya utendaji wao.

Kuhusu adhabu kwa vyombo vya habari, Kauthar alisema hilo ni jambo linalohitaji kutazamwa kwa jicho la tatu kwa maslahi ya wengi na taifa kwa jumla.

Alimkariri Waziri wa Habari na Teknolojia Tanzania Nape Nnauye katika hutuba aliyoitoa hivi karibuni kwenye sherehe ya kuadhimisha miaka 60 ya shule kuu ya habari na mawasiliano ya umma ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Katika sherehe hizo, Nape alisema kitendo cha kulifungia gazeti, redio au televisheni pale mwandishi mmoja anapoandika habari potofu dhidi ya mtu au taasisi yoyote, si busara kukifungia chombo cha habari.

“Tuchukulie mfano wa sekta ya afya, iwapo daktari au muuguzi amekiuka maadili, ni yeye ndiye wa kuhukumiwa na haifungiwi hospitali kwani kufanya hivyo kutaathiri wengi zikiwemo familia za wafanyakazi,” alimkariri Waziri Nnauye. 

Mwanamama huyo alikwenda mbali kwa kushauri Zanzibar katika kutanua wigo na kuongeza uhuru wa habari na kujieleza, ifike pahala ikopie utamaduni wa Uingereza, wa kuruhusu watu kutumia eneo la Hyde Park kutoa madukuduku yao bila kuguswa ili mradi tu hawafanyi hivyo nje ya sehemu hiyo. 

 

Alisema ingawa watu wanaweza kutumia fursa hiyo kusema maneno makali, lakini hakutakosekana ushauri wenye tija ambao kamati itakayoundwa kufuatilia uhuru huo wa kujieleza, watayaorodhesha na kuyafikisha serikalini kwa kufanyiwa kazi.

Jumuiya za vyama vya watu wenye ulemavu ni miongoni mwa wadau wa habari, na mwandishi wa makala haya alizungumza na Mratibu Jumuiya ya Watu  Wasioona Zanzibar (ZANAB) kupata maoni yake.

Alikiri kuwa huu ni wakati muafaka Zanzibar ipate sheria mpya ya habari ili kukidhi matakwa ya uhuru wa kujieleza na kuwa na serikali inayoendeshwa kwa misingi ya uwazi na ukweli.

Alifahamisha kwamba, uzoefu unaonesha mara nyingi baadhi ya viongozi wanaviogopa vyombo vya habari labda kwa kuwa miongoni mwao hawako safi kwa asilimia 100.

Alikumbushia kuwa Zanzibar ilikuwa na sheria Namba 5 ya usajili wa wakala wa habari, magazeti na vitabu ya mwaka 1988 ambayo ilionekana na mapungufu yaliyokuwa yakikwamisha haki  ya uhuru wa vyombo vya habari na uandishi wa habari visiwani humu.

Alisema hata baada ya marekebisho hayo imeonekana kuwa bado sheria iliyopo sasa haitekelezeki vizuri.

Alitaja sababu za kutokutekelezeka huko, kuwa ni kutokana na ukweli baadhi ya viongozi hawako tayari kuwapa waandishi taarifa wazitakazo kikamilifu japokuwa zina maslahi kwa umma.

 


“Mbali na kunyimwa habari, vikwazo haviishii hapo, kwani mara kwa mara kumeripotiwa kesi za baadhi ya wanahabari kutishwa, vifaa vyao kuzuiliwa na kupekuliwa, na hata kuwekwa kizuizini kwa madai yanayopambwa rangi za kufanya uchochezi na kuvuruga amani ya nchi,” alifafanua.

Adil alisema kwamba waandishi wa habari ni wadau wa maendeleo, na pia ni jicho linaloona mbali, hivyo kupitia harakati zao wana uwezo mkubwa wa kuibua changamoto mbalimbali pamoja na kupaza sauti za wasiosikika ili kuleta mabadiliko chanya.


Alibainisha kuwa umefika wakati sasa viongozi na watendaji wa sekta za serikali na binafsi wawaone waandishi kuwa ni marafiki badala ya kuwaweka kwenye kundi la maadui.

“Kwa maoni yangu, mtendaji au kiongozi hana haki ya kukidhibiti chombo cha habari au kumuwekea vikwazo mwandishi asitoe taarifa. Dawa hapa ni watendaji wasiotaka kuripotiwa maovu yao ikiwemo wizi wa mali ya umma na rushwa, ni kubadilika na kufuata sheria,maadili na miongozo ya kazi,” alisisitiza.

Alitaka sheria ijayo, iepuke kuwapa viongozi mamlaka makubwa zaidi kuvidhibiti vyombovya habari ikiwemo haki ya kuvifuta.

Aidha alitaka baadhi ya maneno yasitumike kwenye sheria hiyo, ikiwemo neno KUDHIBITI ambalo linajitokeza sehemu nyingi katika sheria ya sasa.

 

Alisema maneno kama hayo pamoja na uwezo uliochupa mipaka kwa wenye mamlaka, yanaweza kutumika vibaya endapo kiongozi atakuwa na chuki binafsi kwa mwandishi au chombo anachokitumikia, au kutegemea anavyoamka.

Alieleza matarajio yake kwamba, sheria mpya inayosubiriwa kwa hamu itakuja kufuta mapungufu yaliyopo na kuweka msingi wa kutumika miaka mingi bila malalamiko na hivyo kuchukua muda mrefu kabla kuibuka haja ya kuipitia na kuirekebisha tena.

Jamila Mahmoud Juma ni Mkurugenzi wa Chama cha Wanasheria Wanawake Zanzibar (ZAFELA), alisema kutokana na maendeleo ya teknolojia yaliyopo sasa, dunia imekuwa wazi na ndogo kufikika, hivyo sheria ijayo ya habari pia izingatie haki ya mtu kupata taarifa kupitia mitandao ya kijamii. 

Alisema ingawa kila mtu anapaswa kufuata  sheria, mabadiliko ya teknolojia yasiachwe kuhalalisha watu kuchafuana, ingawa ni busara mitandao ipewe heshima yake kwa kuwekewa taratibu zinazolinda hadhi ya mtoa na mpokea habari.

“Kudhibiti mitandao na kasi ya upatikanaji taarifa duniani ni jambo gumu kwa sasa, hata hivyo, mamlaka zinapaswa kuweka sheria madhubuti ambazo hazitapendelea upande wowote, bali zitamzindua mtumiaji kifaa cha kielektoniki awe makini kuepuka kumdhuru mtu mwengine,” alisema.

Hata hivyo, alishauri viongozi  wajifunze na kuukubali utamaduni wa kukosolewa hasa inapokuwa mkosoaji/mwandishi amelenga kutetea na kulinda maslahi mapana ya taifa.

 

Alieleza kuwa kukifungia chombo cha haabari au mwandishi hauwezi kuwa ufumbuzi wa tatizo, lakini serikali inapohisi imekosewa au mtu anapoona amekashifiwa,atumiemabaraza ya usuluhishi au hata vyombo vya sheria kutafuta haki.

“Kutokana na utandawazi uliotawala dunia, tukiendekeza mchezo wa kufungiafungia vyombo na waandishi, itafika siku tutaamka asubuhi hakuna hata gazeti moja au vituo vyote vya redio na televisheni vimefungwa. Tusifike huko na sheria ijayo isiweke ugumu kama huo,” alihitimisha.

Baadhi ya wadau waliotoa maoni yao, walishauri Zanzibar itakapofanyia marekebisho Katiba yake iige mfano wa nchi jirani ya Kenya na nyengine kwa kuingiza matakwa ya mkataba wa Afrika Mashariki kuhusu haki za binadamu.

Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Zanzibar (ZU) Dkt. Suleiman Seif Omar, alisema Kenya ilifanya jambo jema kwani katika marekebisho ya Katiba yake yaliyofanywa mwaka 2010, uhuru wa kujieleza na kupata habari umepewa umuhimu na uzito  unaostahili katika Ibara za 33, 34 na 35.

 

“Kwa mfano Ibara ya 33 (2) imesisitiza kuwepo uhuru wa kuendesha vyombo vya habari vya kielektroniki, vya uchapishaji na aina nyengine zote za vyombo vya habari,” alitoa mfano.

Kilichomkuna zaidi, ni Ibara hiyo inaposema, “Serikali haitapaswa; (state shall not);

 

-Kudhibiti au kuingilia mtu yeyote anayejishughulisha na utangazaji, utoaji au usambazaji wa uchapishaji wowote au usambazaji wa habari kwa chombo chochote”. Aidha;

 

Kuadhibu mtu yeyote kwa maoni au mtazamo wowote au maudhui ya matangazo yoyote, uchapishaji au usambazaji.

 

Eneo jengine alilovutiwa nalo ni ;

 

33(3) Utangazaji na vyombo vyengine vya habari vya kielektroniki vina uhuru wa kuanzishwa, kwa kuzingatia tu taratibu za leseni ambazo;

(a) Nii muhimu kudhibiti mawimbi ya hewa na aina nyenginezo za usambazaji wa mawimbi; na

(b) Havipaswi kudhibitiwa na serikali, maslahi ya kisiasa au maslahi ya kibiashara.

 

33(4) Vyombo vyote vya habari vinavyomilikiwa na Serikali vitakuwa;

(a) Huru kuamua kwa uhuru maudhui ya uhariri wa matangazo yao au mawasiliano mengine;

(b) Kutokuwa na upendeleo; na

(c) Kutoa fursa ya haki kwa uwasilishaji wa maoni tofauti na maoni yanayopingana.

 

Hata hivyo, Dkt. Seif ambaye ni Meneja wa zamani wa Baraza la Habari Tanzania (Zanzibar), alitoa tahadhari kwamba pamoja na kutaka sheria mpya ya habari isiyokuwa ngumu, alikumbusha wajibu wa wanahabari kuzingatia taarifa zinazojenga zaidi badala ya zile zinazochochea vurugu na mifarakano.

 

“Ni haki yetu kudai sheria yenye mazingira rafiki kwa kazi zetu,lakinini wajibu wetu pia kukumbuka usalama wanchi yetu na kujitahidi kalamu na kamera zetu zisiwe chanzo cha mifarakano na kusambaratisha taifa kwani likizama tutaangamia sote,” aliweka kituo.

 

 

 

 

 

 

 

Comments

BLOG'S VISITORS

DAKTARI MWENGINE CHAKE CHAKE KULA SIKUKUU POLISI, NI KWA TUHUMA ZA KUMBAKA MGONJWA WAKE

NA WAANDISHI WETU, PEMBA::: DAKTARI anaetoa huduma kwa wagonjwa kituo cha afya cha serikali cha  Gombani wilaya ya Chake Chake Pemba, Is-haka Rashid Hadid, anaendelea kushikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa kaskazini Pemba, akituhumiwa kumtorosha na kisha kumbaka mtoto wa mwenye umri wa miaka 16, mkaazi wa Gombani. Daktari huyo miaka 35 ni mkaazi wa Kangagani Wilaya ya Wete mkoani humo, ambapo anadaiwa alimchukua mtoto huyo kutoka kwa rafiki yake, na kumpeleka kwenye nyumba anayoishi eneo la Kangagani. Mtoto aliefanyiwa kitendo hicho alisema kuwa, April 21 mwaka huu alikwenda kituo cha afya Gombani, kwa ajili ya matibabu na baada ya kupatiwa huduma na daktari huyo, alimuomba nambari yake ya simu. Alisema ilipofika usiku, walikuwa wanawasiliana kupitia ujumbe mfupi (sms) kwa lengo la kwenda kuchukua dawa nyingine ambazo kwa mchana huo alizikosa hospitalini hapo. "Nilikwenda hospitali kutibiwa, baada ya kufanya mapele katika sehemu zangu za siri, lakini akaniambia mpaka aje da

'MKAPA' NA WENZAKE PEMBA WALAZWA RUMANDE

  NA HAJI NASSOR, PEMBA@@@@ MAHKAMA kuu Zanzibar kisiwani Pemba, chini ya Jaji Ibrahim Mzee Ibrahim, imewapeleka rumande watumuhimwa wanne wanaokabiliwa na tuhuma za kuua kwa makusudi, akiwemo Ali Mussa Omar ‘ Mkapa’ mkaazi wa Wawi wilaya ya Chake chake Pemba. Watuhumiwa wengine walioanza maisha mapya ya rumande ni mtuhumiwa Yassir Mohamed Juma miaka 23, Anuwari Mussa Omar miaka 30 pamoja na mtuhumiwa Yassir Mussa Omar ‘ Makababu ’ miaka 29, wote wakaazi wa shehia ya Wawi, wilaya ya Chake chake Pemba. Awali watuhumiwa hao waliwasili mahakamani hapo, kwa mara ya kwanza, kwa ajili ya kusomewa tuhma zinazowakabili za kumuua kwa maksudi Said Seif Kombo. Ilidaiwa mahakamani hapo na Mwendesha Mashtaka kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashataka Seif Mohamed Khamis akiambatana na mwenzake Mussa Khamis Ali kuwa, watuhumiwa hao kwa pamoja wanadaia kufanya mauwaji hayo kwa maksudi. Ilidai kuwa, watuhumiwa wote kwa pamoja, walitenda kosa hilo Oktoba 16, mwaka huu, baina ya saa 7:00 mchan

HII KALI MBUNGE ASIYA AMKOGESHA MWANANCHI HADHARANI KISA HICHI HAPA......

  NA HAJI NASSOR, PEMBA MBUNGE wa viti maalum nafasi za wanawake mkoa wa kaskazini Pemba Asiya Sharif Omar, amewataka wananchi wa kijiji cha taifu, shehia ya Kinyasini jimbo la Gando wilaya ya Wete Pemba, kuyalinda miundombinu ya maji safi na salama, ili yawe endelevu kwao. Kauli hiyo ameitoa wakati alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi, mara baada ya kuwasili kijijini humo, na kumkogesha mwananchi mmoja kama ishara ya uzinduzi wa mradi wa maji safi na salama, ulioasisiwa na mbunge wa Jimbo la Gando. Alisema, hawana mbadala kwa sasa bali ni kuilinda miundombinu ya huduma hiyo, hasa baada ya mbunge wa wao Salim Mussa Omar, kuwarejeshea huduma hiyo. Alieleza kuwa, inafahamika kuwa kwa miaka 14 waliikosa huduma hiyo hasa kwa vile viongozi waliokuwepo hawakujali kuwatatulia tatizo hilo, hadi juzi ilipofanywa na mbunge wao. “Baada ya huduma hii sasa kurejeshwa na mbunge wa jimbo la Gando, kazi iliyobakia kwenu wananchi ni kila mmoja kuwa mlinzi wa miundombinu hii,’’ali

TUHMA ZA DAKTARI PEMBA KUCHIWA HURU: POLISI KASKAZINI KUTOA TAARIFA RASMI LEO

  NA HAJI NASSOR, PEMBA KAMANDA wa Polisi mkoa wa kaskazini Pemba, Juma Saad Khamis, amesema leo Mei 9, mwaka huu atatoa taarifa rasmi, juu ya kuendelea kumshikilia au kumpa dhamana ya Polisi, daktari wa Kituo cha Afya Gombani Is-haka Rashid Hadid, anayetuhumiwa kwa ubakaji. Alisema, kwa vile alikuwa katika mapumziko mafupi, haelewi jambo lolote linaloendelea kwa mtuhumiwa huyo, juu ya kuendelea kushikiliwa kwake kituoni hapo. Alieleza kuwa, leo Mei 6 (jana), hajapata taarifa za ndani za mtuhumiwa, huyo na kuwataka wananchi na wanaharakati, wasubirie hadi Jumatatu ijayo. Akizungumza na waandishi wa habari kwa nyakati tofauti Kamanda huyo, alisema hana taarifa zozote za kupewa dhamana mtuhumiwa ndani ya kituo chake cha Polisi au kuendelea kuwepo. ‘’Ilikuwa mimi sipo kazini kwa muda, kuanzia anakamatwa hadi anafikishwa Polisi, kwa sasa siwezi kueleza jambo lolote kwa mtuhumiwa huyo, hadi Jumatatu,’’alieleza. Aidha Kamanda huyo alieleza kuwa, kwa sasa hawezi kutoa ufafan

MADAKTARI KUTOKA CHINA WAOKOA MAISHA YA MTOTO PEMBA

  HABIBA ZARALI, PEMBA TIMU ya 32 ya madaktari wa kichina katika hospitali ya Abdalla Mzee Mkoani wamefanikiwa kufanya upasuaji mkubwa wa mtoto mwenye umri wa miaka 15 mkaazi wa Chole Kengeja, baada ya kuchomwa na jiti sehemu ya njia zake za mfumo wa uzazi. Mtoto huyo ambae alianguka hivi karibuni katika mti na baadae kuchomwa na jiti hilo na kumsababishia kutokwa na damu nyingi katika sehemu ya nyonga, alifanyiwa upasuaji uliodumu kwa muda wa saa tatu na   kuokolewa maisha yake. Akizungumza mara baada ya operesheni huo kiongozi wa timu hiyo Dr Jiang Jinhua, alisema mara baada ya mtoto huyo kufikishwa hospitalini hapo na kufanyiwa vipimo na kuonekana   ilibidi apatiwe rufaa ya kwenda katika hospitali nzuri yenye kutibu tatizo lake huko nchini Kuwado ambapo haikuwezekana kutokana na hali ya umaskini wa f amilia ya mtoto huyo . Alisema timu ya madaktari hao itaendelea kutowa huduma za matibabu   kwa wananchi kisiwani humo,   ili kuwaondolea gharama ya kutafuta matibabu nje ya nch